Post by Yona Maro on Dec 11, 2005 6:34:19 GMT -5
UCHAFUZI na uharibifu wa mazingira ambao kwa kiasi kikubwa hutokana na shughuli za binadamu, unahatarisha mustakabali wa uhai duniani. Makala hii ya BBC News Online iliyotafsiriwa na MWESIGA MULINDA inabainisha baadhi ya masuala muhimu ya kimazingira yanayohatarisha uhai wa binadamu na viumbe wengine.
BINADAMU ni spishi (species) iliyofanikiwa zaidi miongoni mwa viumbe hai wote, kiasi cha kuitawala dunia, huku kasi ya maendeleo yake ikiongezeka siku hadi siku.
Kwa kuzingatia maendeleo ambayo yamekuwa yakipatikana hatua kwa hatua, wataalamu wamekuwa wakitaja zama mbalimbali ambazo binadamu wamezipitia hadi kufikia hapa walipo, kuanzia zama za mawe, zama za chuma, hadi zama hizi za sayansi na teknolojia.
Hata hivyo, pamoja na zama tulizo nazo sasa kufahamika kama zama za sayansi na teknolojia, wataalamu wanasema hizi pia ni zama za binadamu kuitawala zaidi na kuitiisha dunia. Wanaziita zama hizi kuwa 'Anthropocene Age'.
Pamoja na sifa hizi ambazo binadamu amejipa katika suala zima la kuitawala dunia, wanasayansi mbalimbali wana wasiwasi kuwa binadamu tumefikia mahali tunahatarisha si tu mustakabali wetu, bali pia mustakabali wa uhai duniani, kutokana na jinsi tunavyoharibu mazingira yetu.
Katika shughuli zetu za kila siku, binadamu tumekuwa tukikabiliana na matatizo mbalimbali, lakini katika zama hizi matatizo tunayokumbana nayo yamekuwa magumu zaidi kuliko katika kipindi kingine chochote. Baadhi ya matatizo hayo hayana suluhisho kamwe.
Yapo mambo kadhaa ambayo yanaweza kujadiliwa katika suala zima la mustakabali wa dunia na viumbe hai walio ndani yake. Lakini katika makala haya yatazungumziwa mambo sita ambayo wataalamu wanakubaliana kuwa ndiyo yanayokumbwa na mgogoro mkubwa zaidi.
Chakula
Katika zama hizi, inakadiriwa na watafiti kuwa mtu mmoja katika kila watu sita duniani kote (sawa na zaidi ya watu bilioni moja) anakabiliwa na tatizo la njaa na utapiamlo, huku jitihada za kuzalisha zaidi ili kukabiliana na hali hii zikikwama kutokana na kuendelea kupungua kwa ardhi inayofaa kwa kilimo.
Maji
Takwimu za kimataifa zinaonesha kuwa ifikapo mwaka 2025, theluthi mbili ya wakazi wa dunia watakuwa wanaishi katika maeneo yenye uhaba mkubwa wa maji na hata wengine wanadiriki kusema mapigano baina ya mataifa katika miaka hiyo mengi yatasababishwa na kugombea maji.
Nishati
Mafuta (petroli) ambayo ndiyo chanzo kikubwa cha nishati duniani kwa sasa, yanatarajiwa kuzalishwa kwa wingi zaidi katika miaka michache ijayo, kiasi kwamba kufikia mwaka 2010, yaani miaka mitano ijayo yatakuwa hayawezi tena kutosheleza mahitaji ya dunia.
Mabadiliko ya hali ya hewa
Kwa mujibu wa Waziri Mkuu wa Uingereza, Bw. Tony Blair, changamoto kubwa zaidi ya kimazingira inayoikumba dunia kwa sasa ni mabadiliko ya hali ya hewa ambayo yatasababisha majanga kama vile ukame, mafuriko, dhoruba kama ile ya tsunami, njaa na kupotea kwa spishi mbalimbali za viumbe.
Bioanuai
Wanasayansi wengi wanaamini kuwa, kutokana na mvurugiko wa bioanuai--yaani uhusiano baina ya viumbe na mazingira--dunia sasa iko katika hatua za mwanzo za kutoweka kwake.
Uchafuzi wa mazingira
Kemikali za hatari zinapatikana kila mahali, ikiwa ni pamoja na ndani ya miili ya watoto wachanga ambao hawajala wala kunywa kitu. Inakadiriwa kuwa mtu mmoja kati ya wanne, sawa na robo ya wakazi wote wa dunia, wanakabiliwa na hatari ya kuvuta hewa iliyochafuliwa na kemikali.
Mambo haya sita yanahusiana na yote ni nyeti, kwa sababu hiyo, hata wanasayansi na watetezi wa mazingira wanashindwa kueleza ni lipi lianze kutekelezwa kabla ya jingine.
Mathalani, ni ajabu kujitahidi kulinda spishi za wanyama na viumbe wengine pamoja na makazi yao ya asili, iwapo mabadiliko ya hali ya hewa yatakuja kuziharibu spishi hizo, au kutengeneza mazao mbadala kwa ajili ya kukabiliana na njaa kama hakuna maji ambayo ni msingi wa uhai.
Lakini tatizo jingine ambalo linahusika sana na mambo yote sita, ni idadi ya watu wanaoikalia dunia. Hivi sasa tayari wakazi wa dunia wamezidi bilioni sita na kwa kuzingatia kasi ya ongezeko la watu Umoja wa Mataifa unasema dunia itakuwa na wakazi wapatao bilioni 8.9 ifikapo mwaka 2050.
Kutokana na hali hiyo, pamoja na kwamba kwa uwiano idadi ya watu maskini inazidi kupungua duniani, lakini kwa idadi watu maskini wanazidi kuongezeka, kwani ongezeko la watu linazizidi nguvu jitihada za binadamu za kujitafutia maendeleo na ustawi.
Umaskini ni mojawapo ya matatizo makubwa ya dunia, kwani huwaacha watu wengi wakiwa hawana chaguo zaidi ya kuharibu mazingira yao. Zaidi ya hapo, umaskini husababisha adha katika maisha na kupunguza wastani wa umri wa wakazi wa eneo husika.
Mtanziko unaoikumba dunia
Kutokana na hali hiyo, hata makala hii itazungumzia zaidi maswali kuliko majibu, utakapofika wakati wa kuyachambua mambo yaliyoelezwa hapo juu moja baada ya jingine.
Mathalani, je, ni watu wangapi katika nchi zinazoendelea wanaoweza kuishi maisha ya matumizi makubwa kama ya wakazi wa nchi zilizoendelea za Kaskazini mwa dunia? Je, hao wengine wanaosalia watakuwa wapi?
Je, tunawezaje kutarajia watu maskini kuheshimu na kulinda mazingira wakati ambapo wanatarajiwa kuyatumia mazingira yanayowazunguka kwa ajili ya kuishi?
Je, maisha yanayozingatia uhifadhi wa mazingira ni starehe kwa matajiri au kitu cha lazima kwa wakazi wote wa dunia ambao kuathirika kwa mazingira kunahatarisha mustakabali wao na vizazi vyao?
Tatizo linaloonekana machoni pa watetezi wa mazingira ni kwamba si wengi wanaojali mustakabali wa dunia hii, hasa kuhusiana na maisha ya vizazi vijavyo.
Leo hii, kwa kuzingatia takwimu za mashirika ya maendeleo, watu wanaoishi maisha mazuri na ya kiafya wameongezeka duniani na kwa kiasi kikubwa wastani wa miaka ya kuishi umeongezeka. Kwa nchi zilizo nyingi, kuna matarajio kuwa hali ya maisha ya wananchi itazidi kuwa nzuri siku hadi siku.
Hata hivyo, wataalamu na watetezi wa mazingira wanasisitiza kuwa imetupasa kutafakari na kutathmini kile tunachokiita mafanikio, ili kuangalia udhaifu unaoambatana na mafanikio hayo, ambao unaweza kutugharimu mustakabali wetu.
Changamoto inayotukabili si kujisikia kusutwa na nafsi zetu kutokana na uharibifu ambao tayari umefanyika, au kuyaenzi mafanikio tunayojivunia, bali ni kutambua kuwa sisi kama binadamu, ama tutaokoka au kungamia kutokana na uharibifu tuufanyao katika sayari yetu.
Teknolojia inazidi kutoa matumaini ya mustakabali mwema wa dunia siku hadi siku. Lakini wachambuzi wa mambo wanasema maendeleo ya sayansi na teknolojia mpaka sasa yameshindwa kuwanusuru watoto 30,000 walio chini ya umri wa miaka mitano ambao hufa kila siku kutokana na njaa na magonjwa yanayoweza kuzuilika.
Kukabiliana na changamoto hizi kuu sita--na ya saba ya ongezeko la watu lisilowiana na maendeleo--ni mambo ambayo binadamu anapaswa kukabiliana nayo kufa na kupona.
BINADAMU ni spishi (species) iliyofanikiwa zaidi miongoni mwa viumbe hai wote, kiasi cha kuitawala dunia, huku kasi ya maendeleo yake ikiongezeka siku hadi siku.
Kwa kuzingatia maendeleo ambayo yamekuwa yakipatikana hatua kwa hatua, wataalamu wamekuwa wakitaja zama mbalimbali ambazo binadamu wamezipitia hadi kufikia hapa walipo, kuanzia zama za mawe, zama za chuma, hadi zama hizi za sayansi na teknolojia.
Hata hivyo, pamoja na zama tulizo nazo sasa kufahamika kama zama za sayansi na teknolojia, wataalamu wanasema hizi pia ni zama za binadamu kuitawala zaidi na kuitiisha dunia. Wanaziita zama hizi kuwa 'Anthropocene Age'.
Pamoja na sifa hizi ambazo binadamu amejipa katika suala zima la kuitawala dunia, wanasayansi mbalimbali wana wasiwasi kuwa binadamu tumefikia mahali tunahatarisha si tu mustakabali wetu, bali pia mustakabali wa uhai duniani, kutokana na jinsi tunavyoharibu mazingira yetu.
Katika shughuli zetu za kila siku, binadamu tumekuwa tukikabiliana na matatizo mbalimbali, lakini katika zama hizi matatizo tunayokumbana nayo yamekuwa magumu zaidi kuliko katika kipindi kingine chochote. Baadhi ya matatizo hayo hayana suluhisho kamwe.
Yapo mambo kadhaa ambayo yanaweza kujadiliwa katika suala zima la mustakabali wa dunia na viumbe hai walio ndani yake. Lakini katika makala haya yatazungumziwa mambo sita ambayo wataalamu wanakubaliana kuwa ndiyo yanayokumbwa na mgogoro mkubwa zaidi.
Chakula
Katika zama hizi, inakadiriwa na watafiti kuwa mtu mmoja katika kila watu sita duniani kote (sawa na zaidi ya watu bilioni moja) anakabiliwa na tatizo la njaa na utapiamlo, huku jitihada za kuzalisha zaidi ili kukabiliana na hali hii zikikwama kutokana na kuendelea kupungua kwa ardhi inayofaa kwa kilimo.
Maji
Takwimu za kimataifa zinaonesha kuwa ifikapo mwaka 2025, theluthi mbili ya wakazi wa dunia watakuwa wanaishi katika maeneo yenye uhaba mkubwa wa maji na hata wengine wanadiriki kusema mapigano baina ya mataifa katika miaka hiyo mengi yatasababishwa na kugombea maji.
Nishati
Mafuta (petroli) ambayo ndiyo chanzo kikubwa cha nishati duniani kwa sasa, yanatarajiwa kuzalishwa kwa wingi zaidi katika miaka michache ijayo, kiasi kwamba kufikia mwaka 2010, yaani miaka mitano ijayo yatakuwa hayawezi tena kutosheleza mahitaji ya dunia.
Mabadiliko ya hali ya hewa
Kwa mujibu wa Waziri Mkuu wa Uingereza, Bw. Tony Blair, changamoto kubwa zaidi ya kimazingira inayoikumba dunia kwa sasa ni mabadiliko ya hali ya hewa ambayo yatasababisha majanga kama vile ukame, mafuriko, dhoruba kama ile ya tsunami, njaa na kupotea kwa spishi mbalimbali za viumbe.
Bioanuai
Wanasayansi wengi wanaamini kuwa, kutokana na mvurugiko wa bioanuai--yaani uhusiano baina ya viumbe na mazingira--dunia sasa iko katika hatua za mwanzo za kutoweka kwake.
Uchafuzi wa mazingira
Kemikali za hatari zinapatikana kila mahali, ikiwa ni pamoja na ndani ya miili ya watoto wachanga ambao hawajala wala kunywa kitu. Inakadiriwa kuwa mtu mmoja kati ya wanne, sawa na robo ya wakazi wote wa dunia, wanakabiliwa na hatari ya kuvuta hewa iliyochafuliwa na kemikali.
Mambo haya sita yanahusiana na yote ni nyeti, kwa sababu hiyo, hata wanasayansi na watetezi wa mazingira wanashindwa kueleza ni lipi lianze kutekelezwa kabla ya jingine.
Mathalani, ni ajabu kujitahidi kulinda spishi za wanyama na viumbe wengine pamoja na makazi yao ya asili, iwapo mabadiliko ya hali ya hewa yatakuja kuziharibu spishi hizo, au kutengeneza mazao mbadala kwa ajili ya kukabiliana na njaa kama hakuna maji ambayo ni msingi wa uhai.
Lakini tatizo jingine ambalo linahusika sana na mambo yote sita, ni idadi ya watu wanaoikalia dunia. Hivi sasa tayari wakazi wa dunia wamezidi bilioni sita na kwa kuzingatia kasi ya ongezeko la watu Umoja wa Mataifa unasema dunia itakuwa na wakazi wapatao bilioni 8.9 ifikapo mwaka 2050.
Kutokana na hali hiyo, pamoja na kwamba kwa uwiano idadi ya watu maskini inazidi kupungua duniani, lakini kwa idadi watu maskini wanazidi kuongezeka, kwani ongezeko la watu linazizidi nguvu jitihada za binadamu za kujitafutia maendeleo na ustawi.
Umaskini ni mojawapo ya matatizo makubwa ya dunia, kwani huwaacha watu wengi wakiwa hawana chaguo zaidi ya kuharibu mazingira yao. Zaidi ya hapo, umaskini husababisha adha katika maisha na kupunguza wastani wa umri wa wakazi wa eneo husika.
Mtanziko unaoikumba dunia
Kutokana na hali hiyo, hata makala hii itazungumzia zaidi maswali kuliko majibu, utakapofika wakati wa kuyachambua mambo yaliyoelezwa hapo juu moja baada ya jingine.
Mathalani, je, ni watu wangapi katika nchi zinazoendelea wanaoweza kuishi maisha ya matumizi makubwa kama ya wakazi wa nchi zilizoendelea za Kaskazini mwa dunia? Je, hao wengine wanaosalia watakuwa wapi?
Je, tunawezaje kutarajia watu maskini kuheshimu na kulinda mazingira wakati ambapo wanatarajiwa kuyatumia mazingira yanayowazunguka kwa ajili ya kuishi?
Je, maisha yanayozingatia uhifadhi wa mazingira ni starehe kwa matajiri au kitu cha lazima kwa wakazi wote wa dunia ambao kuathirika kwa mazingira kunahatarisha mustakabali wao na vizazi vyao?
Tatizo linaloonekana machoni pa watetezi wa mazingira ni kwamba si wengi wanaojali mustakabali wa dunia hii, hasa kuhusiana na maisha ya vizazi vijavyo.
Leo hii, kwa kuzingatia takwimu za mashirika ya maendeleo, watu wanaoishi maisha mazuri na ya kiafya wameongezeka duniani na kwa kiasi kikubwa wastani wa miaka ya kuishi umeongezeka. Kwa nchi zilizo nyingi, kuna matarajio kuwa hali ya maisha ya wananchi itazidi kuwa nzuri siku hadi siku.
Hata hivyo, wataalamu na watetezi wa mazingira wanasisitiza kuwa imetupasa kutafakari na kutathmini kile tunachokiita mafanikio, ili kuangalia udhaifu unaoambatana na mafanikio hayo, ambao unaweza kutugharimu mustakabali wetu.
Changamoto inayotukabili si kujisikia kusutwa na nafsi zetu kutokana na uharibifu ambao tayari umefanyika, au kuyaenzi mafanikio tunayojivunia, bali ni kutambua kuwa sisi kama binadamu, ama tutaokoka au kungamia kutokana na uharibifu tuufanyao katika sayari yetu.
Teknolojia inazidi kutoa matumaini ya mustakabali mwema wa dunia siku hadi siku. Lakini wachambuzi wa mambo wanasema maendeleo ya sayansi na teknolojia mpaka sasa yameshindwa kuwanusuru watoto 30,000 walio chini ya umri wa miaka mitano ambao hufa kila siku kutokana na njaa na magonjwa yanayoweza kuzuilika.
Kukabiliana na changamoto hizi kuu sita--na ya saba ya ongezeko la watu lisilowiana na maendeleo--ni mambo ambayo binadamu anapaswa kukabiliana nayo kufa na kupona.